TATIZO LA KUZIBA KWA MIRIJA YA MKOJO

Lifahamu tatizo la kuziba kwa mrija wa mkojo







Mrija wa mkojo (urethra) ni kiungo muhimu kinachotoa mkojo nje ya mwili kutoka

kwenye kibofu. Mrija huu unaposinyaa au kuziba hufanya utokaji wa mkojo kuwa wa

mashaka na maumivu makubwa. Kusinyaa/ Kuziba kwa mrija wa mkojo huitwa pia

urethral stricture.



Visababishi na vihatarishi vya tatizo hili



Kusinyaa kwa mrija wa mkojo husababishwa na kovu linalotokea katika sehemu ya

mrija baada ya mtu kuumia, kufanyiwa upasuaji au kupona magonjwa ya zinaa.



Inaweza pia kusababishwa na uvimbe karibu na eneo la kinena unaokandamiza mrija.

Vihatarishi vya tatizo hili ni pamoja na



 Kuwa na historia ya kuugua magonjwa ya zinaa



 kuwahi kuwekewa mipira ya mkojo au vifaa vya namna hiyo (catheter au

cystoscope)



- Kuvimba tezi dume (BPH) kwa wanaume

- Kuwa na historia ya kuumia au kupata majeraha maeneo ya kinena. Hii hutokea

sana kwa wale wanaopata ajali wakiendesha baiskeli

- Kupata maambukizi ya mara kwa mara ya mrija wa mkojo (urethritis)

- Ni nadra sana kwa tatizo hili kutokea kwa wanawake. Aidha ni nadra pia kwa

mtoto kuzaliwa akiwa na tatizo hili (congenital urethral stricture).



Dalili za tatizo hilo.



Mtu mwenye tatizo hili anaweza kuwa na dalili zifuatazo,

- Kutoa shahawa zilizochanganyika na damu.

- Kukojoa mkojo mweusi au uliochanganyika na damu.

- Kupungua kwa kiasi cha mkojo kinachotolewa.

- Kukojoa kwa shida.

- kutoa uchafu katika mrija wa mkojo.

- kukojoa mara kwa mara.

- Kushindwa kumaliza mkojo wote.

- Kushindwa kuhimili kutoka kwa mkojo (mkojo kujitokea wenyewe/kujikojolea).

- Maumivu wakati wa kukojoa.

- Maumivu chini ya tumbo.

- Maumivu ya kinena

- Mtiririko dhaifu wa mkojo (hutokea taratibu au ghafla)

- Mkojo kutawanyika ovyo wakati wa kukojoa

- Kuvimba uume



Uchunguzi

Daktari atakufanyia uchunguzi wa mwili na namna unavyokojoa. Uchunguzi wa mwili

unaweza kuonesha:



-Kupungua kwa mkondo wa mkojo

- Uchafu kutoka katika mrija wa mkojo

- Kibofu kilichojaa/kuvimba

- Kuvimba kwa mitoki ya maeneo ya kinena

- Tezi dume iliyovimba au yenye maumivu

- Kuhisi kitu kigumu chini ya uume

- Uume kuvimba au kuwa mwekundu

- Hata hivyo, wakati mwingine uchunguzi unaweza usioneshe tatizo lolote lile.



Vipimo



Vipimo ni pamoja na

- Kipimo cha kuchunguza mrija pamoja na kibofu cha mkojo (cystoscopy)

- Kuangalia kiasi cha mkojo kinachobaki katika kibofu baada ya kukojo (Post-void

residual (PVR) volume)

- X-ray ya mrija wa mkojo (Retrograde urethrogram)

- Vipimo vya magonjwa ya zinaa



Matibabu



Mrija unaweza kutanuliwa wakati wa kipimo cha cystoscopy na hiyo ikawa ndiyo

mojawapo ya tiba. Iwapo njia ya kutanua mrija haioneshi mafanikio sana, upasuaji

unaweza kuhitajika. Upasuaji unategemea eneo lilipo tatizo na ukubwa wa tatizo.



Kama tatizo ni dogo/fupi na lipo mbali na bawabu inayotenganisha mrija na kibofu cha mkojo,

linaweza kutatuliwa kwa kukata kasehemu kalikoziba wakati wa kufanya cystoscopy au

kwa kuweka kifaa maalum cha kuzibua na kutanua mrija.



Kama tatizo ni kubwa zaidi, upasuaji wa wazi wa eneo husika unaweza kufanyika.

Upasuaji huu unajumisha kukata sehemu iliyoziba na kisha kukarabati sehemu hiyo.



Kwa mgonjwa ambaye amepata shida ya ghafla ya kushindwa kutoa mkojo (acute

retention of urine), matibabu ya dharura ya kumuwekea catheter kupitia juu ya kinena

(suprapubic catherization) hufanyika. Hii husaidia kibofu kutoa mkojo nje kupitia kwenye

bomba lililowekwa chini ya tumbo.



Ifahamike kuwa mpaka sasa hakuna dawa ya tatizo hili zaidi ya njia za upasuaji na

nyingine zilizoelezwa hapo juu.



Matarajio



Mara nyingi matibabu huleta matokeo mazuri na mgonjwa anaweza kuishi maisha yake

kama kawaida. Hata hivyo wakati mwingine, mgonjwa anaweza kuhitaji matibabu ya

mara kwa mara ili kuondoa sehemu ya kovu iliyopo katika mrija wa mkojo.



Madhara ya tatizo hili



Tatizo hili halina budi kutibiwa haraka maana kama likiachwa linaweza kusababisha

kuziba kabisa kwa njia ya mkojo na kusababisha mkojo kujaa katika kibofu, hali

ambayo, pamoja na kuleta maumivu makali kwa mgonjwa inaweza pia kusababisha figo

kushindwa kufanya kazi (ARF).

Kinga



Ni muhimu kujikinga dhidi ya magonjwa ya zinaa kwa kufanya ngono salama au kuacha

kabisa kufanya ngono. Aidha kuwa makini na kazi au mambo ambayo yanaweza

kukusababishia kuumia maeneo ya kinena







All the best in your health

Comments

Popular posts from this blog

UGONJWA wa Pingili

KUJIFUNGUA KWA OPERATION

FAIDA YA KAROTI MWILINI